
Dar es Salaam — Equity for Tanzania Limited (EFTA) imeanza mara moja utekelezaji wa matumizi ya mapato yatokanayo na Hati Fungani yake (Corporate Bond) iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), kufuatia kukamilika kwa mchakato wa kupokelewa na kuidhinishwa kwa matokeo ya ofa ya umma.
Tukio la uorodheshwaji wa hati hiyo katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) lilihusisha ishara ya kihistoria ya ufunguzi wa soko, likiambatana na mazingira ya shangwe ya wadau wa masoko ya mitaji, kuashiria mwanzo wa safari mpya ya EFTA katika soko la mitaji la Tanzania. Kengele ya soko ilipigwa kama ishara rasmi ya kuingia kwa dhamana hiyo sokoni, ikionesha imani ya wawekezaji na uimara unaozidi kuimarika wa mfumo wa fedha nchini.
Muda mfupi baada ya hatua hiyo, EFTA imeidhinisha awamu ya kwanza ya ufadhili utakaowanufaisha zaidi ya wakulima 1,500 kupata power tillers pamoja na wakulima zaidi ya 300 kupata matrekta. Hatua hii inaashiria mwanzo wa kuelekeza mtaji wa wawekezaji katika sekta zenye tija ya moja kwa moja katika uzalishaji wa kiuchumi.
Hatua hiyo inatokana na mafanikio ya kuorodheshwa kwa Programu ya Hatifungani ya Muda wa Kati (MTN) – Tranche I ya EFTA, ambayo ilivutia takribani TZS bilioni 33 dhidi ya lengo la awali la TZS bilioni 15, hali inayoonesha usajili kupita kiasi na kuakisi imani kubwa ya wawekezaji katika taasisi hiyo pamoja na uimara wa soko la mitaji nchini.
Akizungumza kuhusu mafanikio hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa EFTA, Bw. Nicomed Bohay, amesema matokeo ya ofa hiyo yanaonyesha mabadiliko muhimu katika namna sekta binafsi inavyoweza kutumia masoko ya mitaji kufadhili shughuli za uzalishaji.
“Usajili kupita kiasi tulioupata unaonesha imani kubwa ya wawekezaji katika mtindo wetu wa biashara na mwelekeo wa soko la mitaji Tanzania. Muhimu zaidi, sasa tunaanza kuona mtaji huu ukifanya kazi moja kwa moja katika uchumi halisi kupitia uwekezaji kwenye kilimo na vifaa vya uzalishaji,” amesema.
Ameongeza kuwa mtaji uliopatikana umeiwezesha EFTA kupanua kasi ya uwekezaji katika kilimo na wafanyabiashara wadogo (SME), ambao ni mhimili muhimu wa kuongeza tija, ajira na uthabiti wa kiuchumi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Bodi ya EFTA, Prof. Andrew Temu, amesema kuorodheshwa kwa hatifungani hiyo ni hatua ya kimkakati kwa taasisi na kwa maendeleo ya soko la mitaji nchini.
“Kuorodheshwa huku ni hatua muhimu sana. Kinaonyesha dhamira ya Bodi kushiriki kikamilifu katika soko la mitaji na kujenga msingi imara wa ufadhili wa muda mrefu unaohitajika kwa ukuaji endelevu,” amesema.
Ameeleza kuwa mafanikio ya programu hiyo yanaakisi utawala bora, ufanisi wa menejimenti, na ulinganifu na malengo ya kitaifa ya kuimarisha masoko ya mitaji kama chanzo mbadala cha ufadhili wa maendeleo.
Prof. Temu pia ameipongeza Capital Markets and Securities Authority (CMSA) pamoja na Dar es Salaam Stock Exchange (DSE) kwa mchango wao katika kuhakikisha mazingira thabiti na ya kuaminika ya uwekezaji.
“Tunapongeza CMSA kwa usimamizi madhubuti na DSE kwa kuendeleza miundombinu ya soko. Hii inaimarisha nafasi ya Tanzania kama kivutio cha uwekezaji na kuonyesha ukomavu wa soko la mitaji,” ameongeza.
Kwa mtazamo wa Bodi, hatifungani hiyo imefanikiwa kufikia malengo muhimu ya kupanua vyanzo vya fedha, kuwezesha uwekezaji wa muda mrefu, na kuimarisha uthabiti wa kifedha wa taasisi.
Bodi imeeleza kuwa itaendelea kusimamia kwa karibu matumizi ya rasilimali, kwa kuzingatia kanuni za utawala bora, usimamizi wa vihatarishi, na vipaumbele vya kimkakati vinavyoleta athari halisi katika uchumi.
EFTA pia imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa soko la mitaji kuhakikisha mafanikio ya awamu ya kwanza ya MTN yanaendelezwa katika matoleo yajayo.
Kwa ujumla, uorodheshwaji wa Corporate Bond ya EFTA unatajwa kama hatua muhimu katika kuimarisha nafasi ya soko la mitaji kama chanzo mbadala cha ufadhili kwa sekta binafsi nchini Tanzania, huku ukichochea uwekezaji wenye tija katika uchumi halisi.


















0 Comments