FAMILIA YAKATAA KUCHUKUA MWILI WA MAREHEMU MOCHWARI, KISA HIKI HAPA
Baba agoma kuchukua mwili wa Marehemu mochwari
MUUNGWANA BLOG / 3 hours ago
Familia ya Isaya Neligwa mkazi wa kata ya Mto wa Mbu, Monduli mkoani Arusha imegoma kuchukua mwili wa kijana wao, Jeremia Neligwa aliyegongwa na gari la polisi Februari 12, mwaka huu
Familia hiyo inataka jeshi la polisi kugharamia kusafirisha mwili wa marehemu kutoka Geita hadi Monduli, pamoja na kulipa gharama za chumba cha kuhifadhia maiti ambazo ni Sh225,000 kwa siku 15 ambazo mwili umekuwa mochwari.
Akizungumza leo (Jumatatu) baba mzazi wa marehemu, Isaya Neligwa amesema hayupo tayari kumzika mwanae Geita na kuliomba jeshi la polisi kuonyesha ushirikiano kwa kumsafirisha marehemu na kulipa gharama za mochwari kwakuwa kifo chake kilisababishwa na mwendokasi wa gari la polisi.
Kamanda wa polisi mkoani Geita, Mponjoli Mwabulambo amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema ilitokea Februari 12 mwaka huu saa 12.30 asubuhi eneo la Mwatulole mjini Geita .
Kamanda Mwabulambo amesema gari ya polisi yenye namba PT 4026 ikiendeshwa na askari Constebo Daniel akiwa katika shughuli zake za kikazi alimgonga Jeremia na kusababisha kifo chake papo hapo.
Mwabulambo ambaye amesema hajapokea malalamiko ya familia hiyo na kuwataka wafike ofisini kwake, amesema jeshi la polisi linamshikilia askari aliyesababisha ajali na kwamba uchunguzi wa polisi unaendelea ili kujua ajali hiyo imesababishwa na uzembe wa mtembea kwa miguu ama wa dereva.
Masengwa blog Ipo Play Store…Download HAPA ,Uwe unapata habari zote kwa urahisi zaidi